Tuesday, September 20, 2016

Taarifa ya TUSHIRIKISHANE kwenye gazeti la HAMASA

Muonekano wake kabla gazeti halijawa printed


Mbunge wa Bukoba Mjini (katikati), Mstahiki Meya wa Manispaa ya Bukoba (kushoto) na Mkurugenzi Mtendaji wa Jamii Media kwa pamoja wakisaini 'MoU
'

 Semina ikiendelea


Washiriki wa semina katika Picha ya pamoja



Hii ni taarifa rasmi iliyochapishwa kwenye Toleo la Pili la Gazeti la Hamasa
Jamii Media, waendeshaji wa mtandao maarufu kwa JamiiForums walikuwa mjini Bukoba kwa siku tatu mfululizo kuanzia Tarehe 3 hadi 5 Agosti, 2016 kwa ziara maalum ya uzinduzi wa Mradi uitwao Tushirikishane.
Mradi huo ambao upo katika hatua ya majaribio una malengo ya kuwasaidia viongozi wa kuchaguliwa na wananchi hususani wabunge kutekeleza ahadi walizotoa wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu uliopita kwa urahisi. Pia mfumo shirikishi unaotumika katika kuendesha Mradi wa Tushirikishane utasaidia Halmashauri kuboresha na kutoa huduma za jamii kwa ufanisi zaidi.
Akiongea mbele la Baraza la Madiwani wa Manispaa ya Bukoba, Mkurugenzi Mtendaji wa Jamii Media na Mwanzilishi-Mwenza wa mtandao wa JamiiForums, Ndg. Maxence Melo aliwashukuru viongozi wa Manispaa ya Bukoba, Madiwani na Mbunge Jimbo la Bukoba Mjini kwa kuupokea mradi wa Tushirikishane na kuonyesha utayari wa hali ya juu katika kushiriki utekelezaji wake.
Aliongeza kuwa, Tushirikishane itatekelezwa katika Majimbo Sita(6) na Jimbo la Bukoba Mjini limekuwa la kwanza kuingia katika hatua ya utekelezaji.
Naye Mbunge wa Bukoba Mjini, Mh. Wilfred Lwakatare alizisifu jitihada za Jamii Media katika kuchochea uwajibikaji hususani kwenye sekta ya umma nchini Tanzania. Aliupongeza ubunifu na dhima iliyomo ndani ya mradi wa Tushirikishane na kuyafananisha maudhui yake na nadharia ya “Usimamizi Lazimishi”
Katika warsha hii, washiriki walikuwa ni kutoka makundi yanayowakilisha wadau wakuu wa mradi; ambayo ni wananchi/wapigakura, viongozi wa kuchaguliwa na uongozi wa Halmashauri wamepata kujua malengo, muundo wa mradi, wajibu wa wadau na jinsi ya kushiriki katika hatua na shughuli mbalimbali za mradi. Pamoja na shughuli hizo, yako matukio mengine makuu mawili yalitendekeka sambamba na warsha hii katika kuelekea kwenye utekelezaji wa mradi.
Washiriki walipata kupitia ahadi zilizotolewa na mgombea aliyeshinda kiti cha Ubunge, jimbo la Bukoba Mjini na kuchagua ahadi kuu tatu kwa umuhimu zinazoweza kutekelezeka ndani ya miezi tisa toka sasa.
Ahadi zilizochaguliwa ni fungu la kwanza linajumuhisha Ujenzi wa Kituo cha Mabasi Kyakailabwa, ujenzi wa Soko-Kuu la Bukoba na soko la Kashai, namba mbili ni kuwawezesha vijana na akinamama kujiajiri kwa kuwapa mikopo ya riba nafuu na mwisho ni kurasimisha makazi na maeneo mapya.
Pamoja na vipaumbele hivi, Mh. Lwakatare na Madiwani walikubaliana kuwahamasisha wakazi wa Jimbo la Bukoba Mjini kujiunga na mifuko ya Bima ya Afya. Suala hili limekubalika kuwa mtambuka na hivyo litakuwa mada ya kudumu katika mikutano ya hadhara na ziara za viongozi.
Warsha ya Tushirikishane ilienda mbali zaidi kwa kuandaaa Mpango-Kazi wa utekelezaji wa ahadi zilizochaguliwa kutekelezwa chini ya usimamizi wa mradi. Ili kuhakikisha pande zote zinazohusika katika Mradi zinatekeleza makubaliano, randama (Memorandum of Understanding) ilisainiwa kati ya Ndugu Maxence Melo, Mkurugenzi Mtendaji wa Jamii Media ambaye atatambulika kama msimamizi na muendeshaji wa mradi, Mh. Wilfred Lwakatare Mbunge Jimbo la Bukoba Mjini - mhusika mkuu katika utekelezaji wa ahadi, na Mstahiki Meya, Chief Karumuna kwa niaba ya Baraza la Halmashauri ya Manispaa ya Bukoba ambalo lina jukumu la kuhakikisha huduma za jamii na Sheria ndogondogo zinaboreshwa.
Jamii Media pia ilimtangaza Mhadhiri Happiness Essau na kumuwezesha kwa kumpatia vitendea kazi vitakachomuwezesha kufanya kazi za Afisa Mawasiliano wa Mradi katika Jimbo la Bukoba Mjini kwa ufanisi. Mhadhiri Happiness atakuwa na jukumu la kukusanya na kusambaza habari zilizothibitishwa juu ya maendeleo ya utekelezaji wa Mpango-Kazi.
Njia zitakazotumika kupashana habari ni pamoja na mitandao ya kiganjani (WhatsApp, Telegram), uzi maalumu kwenye tovuti ya JamiiForums.com, makala kupitia FikraPevu.com, kurasa za mitandao ya Twitter, Facebook, Instagram zinazomilikiwa na Jamii Media na kupitia vyombo vingine vya habari.
Gazeti lako pendwa la HAMASA ni mdau aliyeidhinishwa kutoa taarifa rasmi juu ya maendeleo ya mradi wa Tushirikishane kwa Jimbo la Bukoba Mjini. Wananchi na wadau wenye kiu ya kuiona Bukoba ikipiga hatua kimaendeleo wanakaribishwa kuitumia HAMASA kuonyesha jinsi gani Tushirikishane inaweza kupanuliwa kwa faida kubwa zaidi.
Description: https://ssl.gstatic.com/ui/v1/icons/mail/images/cleardot.gif



- MWISHO -

No comments:

Post a Comment